Ingia / Jisajili

Bernard Mukasa

Mfahamu Bernard Mukasa, mtunzi wa nyimbo za Kanisa Katoliki. Kutoka Jimbo la Dar es Salaam Parokia ya Makuburi

Maelezo zaidi

Idadi ya nyimbo SMN: 232 > Zitazame

Jimbo analofanya utume: Dar es Salaam

Parokia anayofanya utume: Makuburi

Namba ya simu: +255 655 670 785

Soma Historia na maelezo yake hapa

Wasiliana na mtunzi kwa email:


Historia / Maelezo

Tumsifu Yesu Kristo.

Bernard Mwombeki Mukasa anaimba sauti ya nne, kwaya ya Mt. Kizito Parokia ya Mwenyeheri Anuarite - Makuburi, Dar Es Salaam.

Alizaliwa Jumatatu ya tarehe 31 Januari 1977 katika kijiji cha kitongoji cha Mugambaizi, Kijiji cha Byamutemba, kata ya Nsunga, Wilayani Misenyi (wakati huo ikiwa bado sehemu ya Wailaya ya Bukoba Vijijini), Mkoani Kagera, Tanzania.

Wazazi wake ni William Mukasa Bernard (Baba) na Apollonia Kokutekeleza Kashaga (mama). Bernard Mukasa ni mtoto wa nane kati ya watoto 11 wa baba na mama hao.

Alibatizwa siku 12 tu baada ya kuzaliwa kwake, katika kigango cha Mt. Bernard hapo hapo kijijini Byamutemba, Parokia ya Kasambya (sasa imemegwa na kuzaliwa parokia ya Mutukula), Jimbo katoliki la Bukoba. Baba yake wa ubatizo ni Katekista Bernard Mashagala (apumzike kwa amani). Maana yake Bernard Mukasa alibatizwa katika kigango cha Mt. Bernard na akasimamiwa na Bernard kama baba yake wa Ubatizo.

Akiwa anakaribia kutimiza miaka miwili, Bernard Mukasa alihamia Parokia ya Biharamulo jimbo la Rulenge (sasa Rulenge – Ngara) pamoja na wazazi na ndugu zake kwa kukimbia vita ya Kagera (Kati ya Tanzania na Uganda), na akajikuta anakulia huko Biharamulo. Akiwa na umri wa miaka mitatu tu, Januari 1980, Bernard alijiunga na kwaya ya Mt. Cecilia ya hapo Biharamulo kama mwimbaji wa sauti ya tatu, na hapo safari rasmi na ndefu ya utume wake wa uimbaji ikaanza, ambayo baadaye ikazalisha ndani yake mwimbaji, mtunzi wa nyimbo, Mwalimu wa Kwaya, Mkufunzi wa walimu na wa uimbaji, Msanifu wa uimbaji, kiongozi wa Waimbaji katika nafasi mbalimbali, nk, kwa kiwango cha juu.

Kwa neema ya Mungu, mpaka Januari 2020, Bernard Mukasa ameandika takribani nyimbo 2,000. Kati ya Hizo, karibu 1,200 zimerekodiwa katika albamu mbalimbali ndani na nje ya Tanzania. Nyingi zaidi zimerekodiwa na zinaimbwa kwa lugha ya Kiswahili, ingawa kuna chache zimerekodiwa au zinaimbwa kwa lugha asilia za makabila ya nje ya Tanzania kama vile Chichewa na Chiyao nchini Malawi, Bemba nchini Zambia, Lingala huko Demokrasia ya Kongo, na Kirundi nchini Burundi.

Wimbo wa kwanza kabisa kutungwa na Mukasa aliutunga kabla hajajua uandishi wa muziki hivyo haukuwahi kuandikwa. Alikua na umri wa miaka mitano, na hapo alitunga nyimbo kadhaa wa kwanza ukiwa wa Krismas ulioitwa Jongeeni Karibu. Jambo moja la kushangaza ni kwamba licha ya Mukasa kuwa maarufu zaidi kwa utunzi wa nyimbo za kuchangamka, yeye mwenyewe kwa vionjo vyake havutiwi sana na nyimbo hizo. Anapendelea zaidi kusikiliza na kuimba nyimbo za polepole. Sio rahisi kumuuliza Mukasa nyimbo zake anazozipenda sana akataja mojawapo ya nyimbo zake maarufu zilizochangamka kama vile MIMINA NEEMA, YESU NI MWEMA nk. Badala yake Mukasa huvutiwa zaidi na nyimbo za polepole kama vile MSILIE, NIMEMALIZA, na GUSANENI MAJERAHA.

Katika utume wa uimbaji, Mungu amemjalia takribani tuzo tano, ikiwemo tuzo ya KUMBUKUMBU YA KARDINALI RUGAMBWA YA MTUNZI WA WIMBO BORA WA KANISA KATOLIKI (Mwaka 2003), na TUZO YA MUZIKI YA KILIMANJARO (KILIMANJARO MUSIC AWARD) YA MTUNZI BORA WA MUZIKI NCHINI TANZANIA (mwaka 2005).

Bernard Mukasa amebahatika kuwa mwasisi halisi wa kwaya moja mpaka sasa, Kwaya ya Bikira Maria Msaada wa Wakristo (BMW) Parokia ya Biharamulo, Jimbo la Rulenge - Ngara (1995), na baadaye kutunukiwa hadhi ya kuwa "Baba wa Kwaya" wa kwaya hiyo mwaka 2005.

Tena, Kwa Neema ya Mungu, alibahatika kuasisi mifumo mitatu muhimu kwa utume wa uimbaji wa leo nchi Tanzania na Afrika Mashariki:

  1. Mfumo wa utawala wa Kwaya wa kisekta, unaofanya kwaya iongozwe kwa kushirikisha kamati kadhaa hasa kamati kuu, kamati ya ufundi na Liturjia, ya Fedha na Mipango, ya Nidhamu na Mahusiano, na ya Sare na Unadhifu, kamati ya maktaba, nk; mwaka 2000.
  2. Mfumo wa utunzi unaobeba ghani asili kabisa ya Kitanzania ikichanganya na asili ya katikati mwa afrika, mwaka 2000. Hata hivyo, kwa karibu muongo mmoja na robo tatu hivi, mfumo huu ulizua mjadala mkubwa wa wanazuoni wa muziki wa kanisa. Wapo waliouona kuwa unaamsha uhai wa ibada na uhai wa nyimbo na hivyo kukoleza chachu chanya ndani ya kanisa, na wapo waliouona kuwa unaathiri uchaji hasa pale unapotumika kwenye ibada. Mjadala huu mzito na wa muda mrefu ulianza kutulia miaka ya mwishoni mwa 2010s’ pale Baraza la Maaskofu Tanzania lilipotumia katiba mpya ya utume wauimbaji nchini kutolea ufafanuzi wa matakwa ya Mtaguso mkuuwa pili wa Vatikano juu ya aina tatu kuu za ghani zinazokubalika na kanisa, na kutoa miongozo ya mazingira sahihi ya uimbaji.
  3. Mfumo wa utoaji sauti linganifu, zenye nguvu na angavu, unatumia ubanaji wat umbo la mwimbaji ili kuhimili kiwango cha pumzi inayotoka kuipeleka nje sauti; mwaka 2002.


Mwezi Februari mwaka 2006, Bernard Mukasa aliasisi siku ya walimu wa kwaya wa Jimbo kuu la Dar Es Salaam, iliyopewa jina la Tamasha la utume wa uimbaji, ambayo iliwaalika na kuwashirikisha wanakwaya wote hata wasiokuwa walimu. Katika kuasisiwa kwa siku hii, ilikusudiwa kuwadhimishwa kila mwaka Jumamosi ya mwisho kabla ya Kwaresma. Katika kuasisi siku hii, alisaidiwa kwa karibu sana na Mwl. Richard Mloka na Dismas Malya. Lengo kuu lilikuwa kuwaunganisha pamoja walimu wa kwaya wa Dar Es Salaam na polepole wa Tanzania nzima ili hatimaye kuasisi chama cha walimu wa kwaya katoliki Tanzania, kusudi kuboresha mahusiano mema kati yao, hatimaye kuleta umoja ambao baadaye ungeweza kurahisisha uundwaji wa shirikisho la kwaya la kitaifa.

Hata hivyo siku ya Walimu haikuadhimishwa mwaka uliofuata baada ya muasisi wake kuhamia nje ya Dar Es Salaam kikazi. Lakini kwa bahati njema, mwaka 2008 shirikisho la kwaya la Jimbo hilo (SHIKWAKA) liliiboresha siku hiyo na sasa ikawa inaandaliwa na SHIKWAKA kila Jumamosi moja kabla ya Pentekoste. 

Mwaka huo huo 2008, Bernard Mukasa aliasisi Tamasha la kila mwaka la Utume wa Uimbaji kwa Jimbo la Sumbawanga sambamba na sala maalumu ya kuombea utume wa uimbaji ambayo inaimbwa kwa muziki wake maalumu, ambavyo kwa pamoja vilizinduliwa rasmi na Baba Askofu Damiano Kyaruzi. Ingawa mwaka uliofuata Bernard Mukasa alihamia jimbo jingine tena kikazi, tamasha hili limeendelea kuadhimishwa kila mwaka mwezi Januari jimboni Sumbawanga.

Mwaka 2010, Bernard Mukasa aliasisi kundi la mtandao la facebook la wadau wa utume wa uimbaji liitwalo Fr. G.F.KAYETTA ambalo lilikua kwa kasi na kusimama kama kiungo muhimu cha kuwafanya waimbaji wafahamiane na kuwasiliana kwa urahisi zaidi bila kujali mipaka ya kijiografia. Kundi hili lilivuka mipaka ya Tanzania, likawa na wanachama kutoka Tanzania, Kenya, Kongo DR, Malawi, Msumbiji, Madagasca, Peru, na wachache toka nchi za Ulaya. Kundi hili, liliasisi vuguvugu la kuanzishwa kwa shirikisho la Utume wa uimbaji Tanzania, vuguvugu ambalo halikufanikiwa kufikia mwisho huko mtandaoni kwa sababu ya tofauti nyingi za kimitazamo, mpaka miaka sita baadaye pale ambapo vuguvugu hilo lilienea na kufika masikioni mwa mababa wa kanisa, nao wakaamua kulirasimisha vuguvugu hilo kuwa mchakato rasmi wa kikanisa chini ya Baraza la Maaskofu Tanzania. Mchakato huu hatimaye ndiyo uliozaa Utume wa kwaya Katoliki Tanzania (UKWAKATA) mwaka 2018, na Bernard Mukasa akateuliwa na Raisi wa Baraza la Maaskofu kuwa mratibu wa kwanza wa Utume huo.

Aidha, kundi hili la mtandaoni la Fr. Kayeta lilizaa tunda jingine muhimu ambalo ni tovuti ya nyimbo za kanisa za kiswahili, www.swahilimusicnotes.com, miongoni mwa matunda mengine kadhaa. Mtaalamu mwanzilishi wa tovuti hii, Mwana- 4 Kayetta Terence Vusille Silonda, baadaye kwa hiari yake aliikabidhi tovuti hii kwa Baraza la Maaskofu na sasa imekuwa mali ya kanisa kwa ajili ya kuuhudumia utume wa kwaya.

Na baada ya kuunganishwa na Kayetta group na kuwa na mawasiliano ya pamoja, wadau mbalimbali wa utume wa uimbaji waliweza hatimaye kutokea humo kuwasiliana na kuunda makundi mengine kadhaa ya mitandao ya jamii yenye malengo mahsusi zaidi ndani ya utume wa uimbaji. Miongoni mwa makundi hayo ni CATHOLIC MUSICIANS ORGANISATION (CMO), CATHOLIC TANZANIA ORGANISTS, MFUKO WAKUSAIDIANA WA WANAKAYETA, na mengine mengi. Haya yote ni matunda chanya au uzao mwema wa kuasisiwa kwa kundi la Fr. Kayetta Group.

Baadaye, mwaka 2013, Bernard Mukasa aliasisi Tamasha maarufu la kila mwaka lijulikanalo kama TAMASHA LA YESU NI MWEMA (TYM) lililoendeshwa na kwaya ya Mt. Kizito Makuburi kwa miaka 4 ya kwanza. Baadaye kwaya hii ilijihisi kukosa utaalamu wa kutosha wa kuliandaa na kuliendesha, na ukakubaliana na muasisi wa tamasha aendelee kuliendesha mwenyewe. Hivyo kuanzia mwaka 2017 Tamasha hili linamilikiwa na kuendeshwa na kampuni yake binafsi inayojishughulisha na masoko, kampuni ya NIMEONJA PENDO COMMUNICATIONS LTD (NPC).

Mpaka sasa Bernard Mukasa ameshiriki na kurekodi albamu zaidi ya 100 zikiwemo za kusikiliza (audio albums) na za kutazama (Video albums). Miongoni mwa albamu alizosimamia maandalizi yake ni pamoja na:

  1. Mimina Neema – Kizito Makuburi
  2. Safari ya Mbinguni – Benedicto, Oruba (Migori) Kenya
  3. Nyumba ya Roho – Kizito Makuburi
  4. Siri ya Moyo wangu – Kizito Makuburi
  5. Mlipuko wa Sifa – Yuda Thadei Mbeya
  6. Silaha ya Mapambano – Kizito Makuburi
  7. Mungu Yule – Kizito Makuburi
  8. Nani Angesimama – Triple V
  9. Upendo na Ukarimu – Triple V
  10. Mungu – Ledokoska, Kiwanja cha Ndege, Dodoma


Aidha, Bernard Mukasa ameendesha mafunzo maalumu kwa kwaya mbalimbali na kuzijengea mapinduzi makubwa ya kiumbaji na kimfumo. Baadhi ya kwaya hizo baada ya hapo zilipiga hatua kubwa na mpaka sasa zimebaki kuwa miongoni mwa kwaya za mfano. Hizi ni pamoja na Mt. Kizito Makuburi (KMK), Ledokoska - K’ndege Dodoma (BMTL), John Paul - II Mbeya Mjini (JMC), Mt. Cecilia Makuburi, nk. 

Kwaya alizowahi kuimbia ni Pamoja na:

  1. Kwaya ya malaika (kwaya ya watoto misa ya jioni) - Parokia ya Biharamulo, Jimbo la Rulenge - Ngara
  2. Kwaya ya Mt. Cecilia - Parokia ya Biharamulo, Jimbo la Rulenge - Ngara
  3. Kwaya ya YCS Tabora Boys
  4. Bikira Maria Msaada wa Wakristo, Parokia ya Biharamulo, Jimbo la Rulenge - Ngara
  5. Kwaya ya Mt. Fransisco Exaviery - Parokia ya Chang'ombe, Jimbo kuu la Dar Es Salaam
  6. Kwaya ya Mt. Denisi Sebugwao - Parokia ya Kristo Mfalme, Jimbo la Sumbawanga
  7. Kwaya ya Mt. Joseph Mfanyakazi - Parokia ya Ruanda, Jimbo kuu la Mbeya
  8. Kwaya ya Mt. Kizito (KMK) - Parokia ya Makuburi, Jimbo kuu la Dar Es Salaam, ambayo ndiyo kwaya ya maisha yake. Mukasa amebaki mwanakwaya wa kwaya hii tangu alipojiunganayo kwa mara ya kwanza mwaka 1998. Licha ya kuhama kimakazi kwa kipindi fulani, amebaki mwanakwaya mwaminifu wa KMK na mshiriki wa kila alichoweza kushiriki akiwa mbali, na wa moja kwa moja baada ya kurudi tena Dar Es Salaam.


Kimuziki, Bernard Mukasa alianza safari yake kwa kufundishwa muziki nyumbani akiwa na umri mdogo kabisa alipokuwa darasa la kwanza. Mwalimu wake wa kwanza wa Muziki ni kaka yake ambaye kwa sasa ni Padri, Pd. Faustine Binamungu Mukasa s.j, ambaye kwa kiasi fulani alishirikiana na kaka mkubwa zaidi (mzaliwa wa kwanza wa wazazi wake), Mwalimu Patrick Mukasa. Baadaye Mukasa alipojiunga na masomo ya Sekondari katika shule ya sekondari ya wavulana Tabora alijiendeleza kimuziki kwa kujiunga na somo la muziki hapo shuleni chini ya mwalimu Kanyabwoya. Wakati huo pia alikuwa akisaidiwa masomo ya ziada ya muziki toka kwa wanafunzi waliokuwa wamemtangulia vidato, hasa hasa Inoocent Kanubo Mukuyuli, Nyachuma Miyaga na zaidi sana Ndg. Edward Samsoni Kidola.

Hata hivyo, Mukasa hakudumu sana na darasa la Mwl. Kanyabwoya baada ya kuona kama mtaala husika uko nyuma ya kiwango cha ujuzi alichokuwa amekwishakipata, akaamua kutumia nafasi hiyo kusoma sayansi ya kilimo. Jambo hili halikumfurahisha sana Mwl. Kanyabwoya ambaye ndiye alikuwa mkuu wa idara ya muziki, kiasi cha kumtenga Mukasa na fursa mbalimbali za idara hiyo. Kwa bahati njema, kipaji cha Mukasa kilitambulika kwa gwiji wa muziki wa kanisa Pd. Luis Malema Mwanampepo aliyekuwa anafundisha katika seminari kuu ya Kipalapala, ambaye alimpa Mukasa fursa ya kuwa anakwenda kuhudhuria darasa lake kila wikiendi. Kifupi, darasa kuu la muziki kwa Mukasa ni Seminari kuu ya Kipalapala – Tabora kwa Pd. Malema, ingawa yeye hakusoma katika seminari hiyo. Darasa hili lilisaidiwa sana na chama maalumu cha Muziki cha jimbo la Tabora (TAEMO) ambacho wakati huo kilikuwa kiliongozwa na mwenyekiti Frt. John Damasen Zilimu na katibu Frt. Ponsianus Kibobela (wote walikuwa mapadri baadaye).

Baada ya kutoka Tabora, Mukasa aliendelea kujiendeleza kwa nadhalia ya muziki kwa vyanzo mbalimbali, lakini alibahatika kupata kozi maalumu ya vitendo katika chuo cha Chiriku Musiconsult kilichokuwa kikimilikiwa kwa pamoja na waalimu watatu wa Chuo Kikuu cha Dar Es Salaam (Dionizi Mbilinyi, Sabinus Komba na John Mgandu). Mukasa alijiunga na kozi hizi kwa kugharamiwa na kwaya ya Mt. Kizito Makuburi ili akajifunze upigaji wa kinanda kwa kuwa kwa wakati huo kwaya hiyo haikuwa na mpiga kinanda wa uhakika, lakini yeye alipofika huko akabadilisha kozi kimya kimya na kusoma kozi tatu tofauti kabisa ambazo yeye aliamini ndizo hasa zitamjenga kuchangia chachu yenye upekee katika fani hiyo. 

Sababu nyingine iliyomsukuma Mukasa kubadili kozi ni kwa kuwa aligundua kwamba hizo kozi tatu zikiunganishwa pamoja gharama yake ni sawa na ile ya kozi moja tu ya kinanda, kwa sababu watu wengi walikuwa hawajiungi nazo hivyo hazikuwa na soko sana. Kozi ya kwanza ilikuwa ya kanuni na mbinu za uimbaji (Choral Techniques), ya pili ilikuwa ualimu wa kwaya na uimbishaji (Choir mastering), na ya tatu ikawa utiribu (Professional conducting.)

Zaidi ya muziki, Mukasa amekuwa mtu mwenye kupenda kuandika vitabu mbalimbali vya dini, ingawa hajafanya vya kutosha katika eneo hilo. Mpaka Januari 2020 Mukasa ameandika vitabu vitatu ambavyo bado havijachapishwa na kusambazwa (Mungu Yule, Ongoko, na Utume wa Uimbaji), na ameandika kitabu kimoja kilichochapishwa na kusambazwa (Gusaneni Majeraha).

Mbali na kuwa mratibu wa utume wa kwaya Katoliki Tanzania (UKWAKATA) nafasi iliyompa tiketi ya kuwa mjumbe wa Halmashauri ya Walei ya Taifa, Mukasa pia amekuwa mjumbe wa Halmashauri ya Walei ya Jimbo kuu la Dar Es Salaam na Parokia ya Makuburi kwa tiketi ya kuwa katibu wa Halmashauri ya Walei ya Parokia, kifupi katibu wa Parokia.

Baada ya kuajiriwa katika taasisi kadhaa, hatimaye Mukasa amejiajiri kama muasisi na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya ukuzaji Masoko inayoitwa NIMEONJA PENDO COMMUNICATIOS (NPC) ambayo pamoja na mambo mengine inajishughulisha na uwakala wa masoko, ushauri elekezi wa kimasoko, uzalishaji wa bidhaa mbalimbali, usambazaji na ukuzaji wa bidhaa za wengine, vyombo vya habari, usambazaji na ukuzaji wa kazi za muziki, nk. Biashara za NPC zinaweza kufikiwa kwa namba ya simu 0768670785 na barua pepe karibu@nimeonjapendo.co.tz

Miongoni mwa malengo ya hivi karibuni ya kiuchumi ya Mukasa ni pamoja na mkakati wa kuanzisha gazeti litakaloitwa Nimeonja Pendo, Kituo cha Redio na cha TV kwa jina hilo hilo la Nimeonja Pendo.

Kifamilia, Bernard Mukasa amefunga ndoa na mwalimu mwenzake wa kwaya, Matilder Sendwa, na wamejaliwa kupata watoto wanne; Victoria, Vinny, Vivian na Vince. Kwa bahati, watoto wao pia wana uelekeo wa utume wa uimbaji. Wanaimba kama wazazi wao, na tayari mmojawao ni mpiga kinanda. Katika kukuza vipaji vya watoto wao, Bernard Mukasa na Mkewe huimba katika kwaya ya familia inayoundwa na wao na watoto wao, ambayo ilianza ikiitwa TRIPLE V, na baadaye ikaitwa QUADRI’V baada ya kuzaliwa kwa Vince. 

Tumsifu Yesu Kristo.